Thursday, September 16, 2010

Utaombwa ukiomba

1.
Si ubwabwa wala pamba, kinachokosa nyongeza,
Kama wewe uliumbwa, kuumbuka unaweza,
Na mchamba huchambwa, na nuru haiwi giza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
2.
Dunia kome la mimba, yalopita hurejeza,
Yazaliwe kama ndumba, nakala ziloigiza,
Hakuna anayetamba, kaziye kama kucheza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
3.
Nakukanya Mwanakamba,ajizi hulegeza,
Uikaze hino kamba, ulimwengu kukufunza,
Na katu kutojigamba,ushujaa hutoweza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
4.
Tosheka na wako mtumba, mpya waachie wenza,
Kama hauna uvumba, udi poa utafukiza,
Komba kama wanalamba, usitafute nyongeza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
5.
Usimwombe mwana gumba,hauwezi muujiza,
Usipeleke kilemba, Pemba hautokiuza,
Huna chumba, vipi nyumba, hunayo unajikweza ?
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
6.
Warembo wana kasumba, na wengine zimeiza,
Usitafute mchumba, kwa sura ya kupendeza,
Huyo aliyemuumba, vingine kamlemaza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
7.
Usitake lima shamba, maji yasikopitiza,
Na ukifuga mtamba, mila jike kuagiza,
Na mchele wenye pumba, bila kupeta hukwaza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
8.
Usiombe utaombwa, hili mwali nakukataza,
Tosheka nacho kibamba, usitamani mkuza,
Dunia ni komba komba, wengi huwapatiliza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?
9.
Utaombwa ukiomba, je, hayo utayaweza ?
Sio wimbo wa kuimba, mjuzi nakukataza,
Mtoka choo kuchamba, desturi yaagiza,
Utaombwa ukiomba , je, hayo utayaweza ?

No comments: