Sunday, September 26, 2010

Mtunukiwa Nobeli

Yangu lugha Kiswahili, nataka niipepete,
Hadi nipate Nobeli, wenye nasibu nifwate,
Waliokwishatawakali, nikae nao nitete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Naitamani Nobeli, hakika kimeremete,
Kipanuke kiswahili, Afrika wakipate,
Tuzinoe na akili, teknolojia tulete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Ni elimu Kiswahili, hazina kwa dhana zote,
Chekechea chahimili, muhibu kwa fani zote,
Hadi kwenye Uzamili, hata kwa shahada tete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Hauwezi kunakili, lugha ya chuma ulete,
Hao sasa mabahili, wataka tuwe viwete,
Wakishatumaliza mwili, akili zite tekete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Japani wastahili, siri yao tupakate,
Ni kikwao kwa asili, si Kiingereza watete,
China nao ni muhali, lugha nyingine ipete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Norwei ama kweli, milioni nne wote,
Wana chao Kiswahili, lingine usiwasute,
Na sasa sio dhalili, nani juu awakute,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Lugha hii mwanamwali, wanaume watafute,
Itatupa afadhali, mengi sana tuyalete,
Kwa kutumia akili, si kwa kuiga tuvute,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Ninaiona amali, Kiswahili kitakate,
Ila dhoofu wa hali, legelege saa zote,
Wanangoja ufadhili, mapya mhali walete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Nitafanza kulhali, lugha yetu ivukute,
Kinamama na rijali, elimu wote wapate,
Kwa lugha ya Kiswahili, na zingine wazitete,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Hakika ubaradhuli, lugha za watu tufate,
Tunakuwa madalali, kuwapa wengine kete,
Mchina keshawasili, je, ni Kichina tukitete ?
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

Mhindi anahimili, je, ni kIhindi tukivute ?
Mtashindwa pilipili, mbaki mwatema mate,
Sura mkazibadili, wajihi muukung'ute,
Ninakumezea mate, mtunukiwa Nobeli!

No comments: