Saturday, September 18, 2010

Ni wewe ukishakufa

Maongozi yetu gea, isiyoelekezeka,
Wapi tunakoelekea, bado hakijaeleweka,
Kila nikiangalia,yananijaa mashaka,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Mipango yao nazaa,kwangu haijaeleweka,
Miaka yake mamia,huko mimi nitafika,
Umri ninaoujua,wala nusu haujafika,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Yapo ninayoyajua,yanachukua miaka,
Lakini mengi halua,michache yanafanyika,
Ila hatujawastua,wawe watu wa haraka,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Ushindani umepoa,kama umehasika,
Hakuna lakuzimua,yachacha na kuchachika,
Daima yao tabia, mambo husahaulika,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Uono wao wa pua,vipi mbali watafika,
Husifu moja hatua,hali elfu twataka,
Ni watu waliolowa,na rahisi kuridhika,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Haitungoji dunia,mwendo lazima haraka,
Lengo ukijiwekea,kuchelewa si mwafaka,
Ukiweza tangulia,unaondoa mashaka,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Afrika yatitia,wengine kwapambazuka,
Magharibi twapotea,Mashariki tunavuka,
Ila kwa wasiojua,kasumba yawafunika,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Mengi nayafikiria, yangekwishatekelezeka,
Wakubwa watutania,dhamira yao wahaka,
Nazidi yaangalia,nakumwachia Rabuka,
Ni wewe ukishakufa, ndio yatatekelezeka.

Copyright © Sammy Makilla-2010

No comments: