Si sukari si mafuta, naona nalishwa sumu,
Pamoja na huu ukata, yanazidi madhulumu,
Ni wapi nitampata, asiye mwana haramu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Utafiti umetota, idara hazina hamu,
Wapima pasipo mita, utapataje takwimu,
Na njaa inatusuta, wengine kulisha sumu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Hili lataka kuteta, na jopo la wala sumu,
Kila mmoja atweta, kutafuta mdhalimu,
Ingawa njiani twapita, wengine si binadamu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Sukari yameremeta, lakini ndani ni sumu,
Chai unapoipata, yaenda chafua damu,
Viungo hukatakata, na kukutia wazimu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Mafuta wanayoleta, hayafai wanadamu,
Mwilini yanatokota, japo chakula kitamu,
Miili inateketa, na nguvu zinahsimu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Viongozi wanapeta, nyumbani hawali sumu,
Je, hotelini wakipita, hawaipati salamu,
Adhaniaye apepeta, aweza kuwa mdimu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Waume watukeketa, nyumba zinakuwa ngumu,
Vuta nikuvute vita, wali wakitahamimu,
Kazi nyumbani twaleta, chumbani kutokudumu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Viongozi twatafuta, wa kikosi maalumu,
Kuyachekecha mafuta, yaliyojaa haramu,
Madukani wakapita, kuyafanyia hukumu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Usukani wamevuta, kweli watu gurudumu,
Na mkia wanafyata, kwa uzito na ugumu,
Na muda ukishapita, huchomwa nayo kaumu,
Tanzania twala sumu, na rijali si rijali !
Tuesday, September 14, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment