Saturday, September 18, 2010

Maziwa

Nyasa kisha Victoria, Tanganyika nalo pia,
Maziwa umejaliwa, mama yetu Tanzania,
Vipi twanyong'onyea, sababu hatujajua,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Usichana waringia, au umekaukiwa,
Kilio tunacholia, bado hujakisikia,
Mikononi twakufia, nawe watuangalia ?
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Maziwa yanasifiwa, kwenye ramani watia,
Ulaya wanayajua, walikikwishayafuatilia,
Misri inayatumia,Sudani na wao pia,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Ndio wanayoyakamua, au unawakamulia,
Watoto wao wakua, unyafuzi watuvaa,
Utapiamlo balaa, huruma yatuumbua,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Enyi kizazi kipya, hili budi kushangaa,
Wazazi wamepagawa, hawaijui dunia,
Wewe waweza ifaa,lakini haitokufaa,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Ujanja tumezidiwa,hata na wapita njia,
Virutubisho wavua,wavipeleka Ulaya,
Sisi bado twazubaa,tunazijali sheria,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Palestina yafaa, kwenda kutembelea,
Mitaro waichimbua, kilomita kwa mamia,
si maji tu yapitia,hata zana na vifaa,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Chini kwa chini watua, kwa juu hautojua,
Hutoka wakaingia, na vito kuvinyanyua,
Uhai waendelea, waisanifu dunia,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Ninalia Tanznia, mama usiyetimia,
Wengine waangalia,wanao waangamia,
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?
Maziwa umejaliwa,unashndwa kunyonyesha ?

Copyright © Sammy Makilla-2010

No comments: