Wednesday, September 15, 2010

Bawabu

Bawabu ninaumia, lakini navumilia,
Kazi yangu kuning'inia,mlango nikishikilia,
Sitoki ninapokaa,wala sijui kutembea,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Nala nilipojengewa,nalala ninapokaa,
Chini siwezi kukaa,Kusimama nimezoea,
Mchana hunizingua,kufunga na kufungua,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Usiku ninaugua, ninashindwa kupumua,
Zinafungwa zangu mbawa,siwezi kujiachia,
Na nyimbo huniishia,ninabaki nasinzia,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Umbo langu ni sawia,mdogo wala sijakomaa,
Ila nabeba dhiraa,wengine zaweza ua,
Kulalama sijajua,utumwa nimezoea,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Ila ninaingojea, siku ya kwenda tembea,
Kwingine nikakujua, mageni kujionea,
Mathalani Tanzania,mikoa na zake wilaya,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Nataka pia dunia, kusafiri na kujua,
Nifike huko Ulaya,barafu kujionea,
pia na huko Asia,maendeleo kujua,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Magharibi kuwachia,mashariki nikajua,
Pepo zenye manufaa,niweze kusafiria,
Niabiri abiria,hata nisikokujua,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Niione na Russia, na China ya kijamaa,
Kwanini waliukimbia,na sisi twautamia,
Nako kusini Korea,Kaskazini nako pia,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Na Mashariki Ulaya,hali sasa kuijua,
Majengo yaliyojaa,lakini bado kuna njaa,
Na Cuba alikozaliwa,Castro mwana mjamaa,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Niende nako India,pamwe nako Malaysia,
Siri yao kugundua,ufukara kuung'oa,
Na sayansi kuivaa,kuileta nyota ya jaha,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Brazili nako pia,mitambo kuitambua,
Na akili ya kuvumbua,Afrika kujinasua,
Tuache tu kununua,vingine kuvivumbua,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Na askari wa dunia,ninataka kumjua,
Marekani mwenye waa,mtata wa jema kujua,
Nafsi inayemsumbua,mguu anapotia,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

Nijue Australia, na kangaroo pia,
Aidha Scandinavia,theluji ilikojaa,
Weupe wa kweli kujua, nazo mosi familia,
Bawabu ninangojea, siku ya kwenda tembea.

No comments: