Wednesday, September 15, 2010

Tumbo

Tamaa mama wa baa, na baba yake msiba,
Tumbo ujazo twajua, vipi zaidi wabeba,
Au hayo mazoea,ya kuhodhi si kushiba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Mboba wahodhi gunia, hali kushiba kiroba,
Tumnbo unafakamia, huoni hiyo ghiliba,
Huwezi ukachukua,zaidi ya unachobeba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Au sasa ni ngamia, huweza weka akiba,
Nundu utaikwaa,mgongoni kuibeba,
Jangwani usife njaa,japo wabeba mikoba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Kula madai ya njaa,hauli kama wakwiba,
Tumbo lataka chukua,kiasi linachokibeba,
Mashine kukokotoa,unaofaa mraba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Mwili wataka kujaa,kadhalika na haiba,
Kitambi chaoghofya,Kikizidi kwa ukbwa,
Mimba waweza mdhania,yule anayekibeba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Uungwana ni kinaya,japo waweza kushiba,
Zaidi ya inavyotakiwa,hali wengine washiba,
Tosheka cha kutumia,uache pia jazba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Kula utakacho pia, kasma haba na haba,
Mradi kinavutia,na unapata kibaba,
Maisha kushangilia,wala si kama msiba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Acha wenzko kutwaa, kiasi cha wao kushiba,
Usifiche cha kuliwa, uvundo kisije beba,
Ndani huja kukuozea,hili halinayo toba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Choyo daima kimbia, hili huvunja nasaba,
Waliotutangulia,kama vile masahaba,
Hili walilikimbia,hawakukubali ghiliba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Chonyo ni mwana izaya,inda mkaza mjomba,
Jamaa hupelekea,wasitoe marahaba,
Na shikamoo kukataa,japo ni yao swahiba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Israfu nayo kataa,japo una kabakaba,
Wenye shida angalia,uwape chao kibaba,
Na yatima kuwalea,wausahau msiba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

Mwogope mwenye kutoa,kwa mtaji pia riba,
Talanta kuzitumia,kama ilivyo akraba,
Na siku ya kushuhudia,wakiri hata bawaba,
Tumbo kushiba kiroba, mbona wahodhi gunia?

No comments: