Wednesday, September 22, 2010

Ndoa zingine kunyonywa

Ndoa zingine maziwa, huishi wewe kunyonywa,
Miaka inavyozidia, wazidi kuanganywa,
Hata kile kilojaa, huishia kumumunywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Kwa dini au sheria, harusi yenu hufanywa,
Ahadi mtazitoa, mkatae kusengenywa,
Na mafunzo mtapewa, na wazazi mkakanywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Ukweli hujifichua, wakati mnap0ofinywa,
Maslahi kupungua, kila pembe mnaminywa,
Hali zinapotitia, watu rahisi kugawanywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Ndugu na hao jamaa, ya uongo hutawanywa,
Hubakia kuvizia, yatangazwa yasiyofanywa,
Na mitego husambaa, wategwe wasiokanywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Hodari walioamua, milele kutokugawanywa,
Kisha wakajititimua, wasiwe watu wa kunywa,
Fedha kudundulizia, waache tena kunyonywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Kuwekeza wakitua, vinginevyo wakatonywa,
Mke anapoamua, hataki tena kunyonywa,
Mbele akavichukua, huku mume anasonywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Mme chumvi hudaiwa, na chake kikamenywa,
Bahili mke akawa, sio wa kumumunywa,
Mme nguvu hulegea, asitake kutekenywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

Ndoa jambo maridhia, ila pasiwe kunyonywa,
Nikahi kitu murua, mtu asiposengenywa,
Nyumba hujititimua, na watu msipogawanywa,
Ndoa zingine kunyonywa, na huku unadanganywa.

No comments: