Wednesday, September 15, 2010

Ni mimi na wewe

Awali tulishakutana, sijui mahala gani ?
Ukanigea amana, kuniingiza peponi,
Na niliposhtukia, ikawa hauonekani,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Leo nakuona tena, macho yangu hayaamini,
Kitu gani nitanena, uwe mwangu mikononi,
Pembe gani nitabana,niwe nawe faraghani,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Wewe kwangu ni hazina,chemchemi ya imani,
Hawa yako sijaona,mwangu tena maishani,
Afya yangu hunona,ukiwa mwangu moyoni,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Imeitikiwa amina,dunia niliyoghani,
Mtima siwezi kana,njia hii naiamini,
Si mtu wa danadana,mashuti yangu makini,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Nimeuona mwamana,nipe ya kwako yamini,
Waisikia adhana,elekea ibadani,
Kuwa radhi Maulana,mja huitwa peponi,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Yangu hayana laana,namuogopa Manani,
Nasihi yake dhamana,kukutia mikononi,
Uwe shuka kwa bayana, pia nami yumkini,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Furaha yangu kufana,tena hapa duniani,
Kwalo hilo kukazana,uelewe ihwani,
Hakika nitajiiona, hai zaidi natona,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Kwanini nipige kona,hali kuna ushindani,
Nikijageuka tena,uwe hauonekani,
kutakana kukamatana,ukiwachia hatiani,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

Hili sasa ninavuna,vaa pete kidoleni,
Itunze yangu amana,niweke mwako moyoni,
Dunia ni pana sana,isije kutuhadaa,
Ni siku nyingine tena,mimi na wewe peponi!

No comments: