Sunday, September 26, 2010

Siasa zetu nyang'anyi

Siasa zetu nyan'anyi, zinatupora uwezo,
Watawala sio nyinyi, mmefanya pandikizo,
Mmejipa na umwinyi, na kuviweka vikwazo,
Siasa zetu nyang'anyi, zinatupora imani !

Wananchi hamnyang'anyi, ilokuwa yenu tunzo,
Mwawaachia wanyonyi, wapita mfululizo,
Na wala hamuwakanyi, waona kama mchezo,
Siasa zetu nyang'anyi, zinatupora imani !
Eti hawatudanganyi, wakati nyie igizo,
Na wala hamuwasunyi, mnawapa madekezo,
Ugonjwa hamuuponyi, mnaongeza mizozo,
Siasa zetu nyang'anyi, zinatupora imani !

Wananchi ndio mamwinyi, wengineo mikwaruzo,
Ukubwa hawakusanyi, ila kama ni tangaZO,
Na kitu hawakifanyi, kuondoa matatizo,
Siasa zetu nyang'anyi, zinatupora imani !

Nguvu hatuzigawanyi, waziiba mzomzo,
Na nchi haichanganyi, kwa kukosa shinikizo
Maduhuli hatukusanyi, utapiamlo wa mawazo,
Siasa zetu nyang'anyi, zinatupora imani !

Tuache unyang'anyi, watu wawe na uwezo,
Chenu hatuwapokonyi, wala hapana mabezo,
Nchi ni usisi si unyinyi, liote kwenye mawazo,
Siasa zetu nyang'anyi, zinatupora imani !

No comments: