Wednesday, September 15, 2010

Mbunge jimbo ni lako

1.
Mbunge umepotea, mwenzetu hatukuoni,
Siku tulipokuchagua, ulitupa nyingi imani,
Wewe kukutegemea, kutuondoa mashakani,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
2.
Mwisho kututembelea, hatukumbuki ni lini,
Ahadi ukazitoa,zote kwishia mitini,
Kinyongo chaning'inia,nyongo watu tumbueni,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
3.
Habari zimeenea, waishi ughaibuni,
Umukua milionea, tena wa matrilioni,
Umaskini wachukia, utakutumbua ini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
4.
Hewa utakuchafulia, wanuka umasikini,
Huwezi kuvumilia, kuona waso thamani,
Na waziri umekua, sikuzote safarini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
5.
Hakuna tulilopangua, mipango hukubaini,
Halipo lililopotea, kwetu hukuwa na thamani,
Hapana kilichochipua, vilifia ardhini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
6.
Hapo ndipo pa kuanzia, kisha tufike mwishoni,
Tulikupa twachukua, wangung'unika nini ?
Vipi utamwamkua,asiye mwako machoni ?
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
7.
Wananchi watachukua, kilicho mwako mkononi,
Na hili sintowaambia, sioni lina walakini,
Kichochoro 'kitumia, kumejaa barabarani,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
8.
Mvuvi anapovua, samaki huwa kapuni,
Wewe umeshakwapua, vyako viko makwapani,
Usiotee kurejea, hiyo ndoto ya mbeleni,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
9.
Wazee mmeshupaa, mmetufanyia nini,
Magenge mmeyazua,kung'atuka mwahaini,
Juu tutawasanzua,vijana fursa wapeni,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
10.
Wanawake wameamua, kazi kuja waonyesheni,
Haraka pisheni njia, midume msio makini,
Nchi twataka komboa, umalizike uzaini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
11.
Vijana wameamua, kuingia madarakani,
Filamu kutuchezea, si ile ya umaskini,
Ya kuukata kwa sanaa, tushangaze duniani,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!

No comments: