Sasa hamthaminiki, wao wameshatosheka,
Ukwasi si yao miliki, hata sisi tunajengeka,
Wazungu muwataliki, ndoa mpya kufungika,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Uchumi wamehiliki, vigumu wataokoka,
Sasa wawa wazandiki, wageni wadhulumika,
Yakini hawawataki, chanzo hawajakishika,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Kazi zinawadhihaki, masoko yanatoweka,
Bei zinawashtaki, mali ghafi imeruka,
Mishahara haishikiki, mambo yanaharibika,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Uzalishaji mikiki, hakuna kinachotoka,
Wachina watamalaki, Mzungu anatishika,
Azidi uza bunduki, Mhindi anamcheka,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Makaburi ya Hilaki, Ulaya yanachibika,
Ni kweupe Mashariki, Magharibi yashtuka,
Chai isiyoiliki, itaanza kunyweeka,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Nduguze hawawataki, sembuse Waafrika,
Ufaransa tahamaki, Gipsi yalowafika,
Mwingereza hamtaki, Mpolishi kamchoka,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Haya msiyadhihaki, yatakuja kuwafika,
Mzungu haaminiki, hali ikiwa mashaka,
Unakwisha urafiki, uadui kujengeka,
Ikiwa hawawataki, rejeeni Afrika !
Sasa hakieleweki, Ulaya imechafuka,
Mungu bara libariki, warudi waliotoka,
Tujenge mpya milki, kote ikatambulika,
Sunday, September 26, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment