Wednesday, September 15, 2010

Washikeni watu hao

Washikeni watu hao, na mzidi kuwapenda,
Ila ndoto moyo wao, hapa kwetu kuupanda,
Si chungwa ni malimaokwao hawaachi kudanda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Wapi mti uoatao,kwenye yetu miji kenda,
Mmea uchanuao, bila mizizi kutanda,
Na matunda wachumao, kwenye mgongo wa nunda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Ni wahenga wasemao, kizazi kujakifunda,
Ulimwengu mtukwao, ndio ufalme huundwa,
Vigumu waponda chao, kokote kuja kupanda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Mbwani hawa watokwao, tena na mwingi udenda,
Kwa wageni waingiao,na pasenti zawaganda,
Mithili neema yao,ni cha mauti kitanda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Hesabu kila wajao, tunajivalisha sanda,
Ila kwa wachache wao,utu wanaoulinda,
Wengine wahamishao,hawa watu wa kuwinda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Ni mfupi wetu upeo, si wa nyumba bali banda,
Na hao watembeao, macho yao yajipanda,
Waonalo si kioo,bali hali kama chanda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Hawajui wajuao, japo wavaa magwamda,
Mchina kwake salioumeshindwa unda Honda,
Mtabaki mnunuao,wala si watu wa viwanda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Hawa wamchunguao, kwanini haruki kinda,
Si wajua wajuayo, kama kweli hajapinda,
Waso mbawa warukao,chini lazima kudunda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Ndio wajulikanao, wapiganao kwa munda,
Hao hao wachechemeao,kwa shukrani za punda,
Ninasema mtukwao,japo kote mtaranda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

Tanzania nipendayo, maskini wangu nyonda,
Laana yako kilio,kwa fikra za mgando,
Liwapi lako kimbilio,wanapotawala nunda,
Mwisho ndege watapanda, kusanzuka kwenda kwao.

No comments: