Sunday, September 19, 2010

Choo si pipa la taka

Choo lina zake taka, lakini si uchafuzi,
Si mahala pa kuzika, ila pakutaladhahi,
Wengi tunakereheka, yasopaswa matumizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Watupaje takataka, na choo hakiyawezi,
Unatupaje viraka, na vipande vya mavazi,
Mnatutia mashaka,na choo hakipendezi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Kaziye kusetirika, kupunguza uchukuzi,
Pasafi ukaviweka, vilivyo na uchokozi,
Nawe ukapumzika, kuvuta safi pumzi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Wenzetu wanasifika, choo kwao matanuzi,
Chooni akishafika, huwa hafanyi ajizi,
Hakika hupumzika, akawa kitu hawazi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Kwingine si Afrika, chooni wanabarizi,
Hekima zikachmbika, vilokuwa hawawazi,
Na ujumbe wakaweka, uende kwa wateuzi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Yabidi kubadilika, vyoo tupate kuenzi,
Bila'vyo kuheshimika, itakuwa si saizi,
Yapo mengi kufanyika, ili tuipande ngazi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Kama nyumba ni mashaka, makazi ni kama zizi,
Vipi choo kujengeka, vyenye thamani azizi,
Watu watatosheka, kustawisha mizizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Hapa kwetu Afrika, hawawazi viongozi,
Wao wamesharidhika, kwa o vyoo i tailizi,
Sisi kutostaarabika, waona yetu saizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

Wengi wao wanshafika, mengine hawayawezi,
Wabebwa kuzoeleka, wala hawafanyi kazi,
Wananchi wanateseka, wao kwao wabarizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !

No comments: