Choo lina zake taka, lakini si uchafuzi,
Si mahala pa kuzika, ila pakutaladhahi,
Wengi tunakereheka, yasopaswa matumizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Watupaje takataka, na choo hakiyawezi,
Unatupaje viraka, na vipande vya mavazi,
Mnatutia mashaka,na choo hakipendezi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Kaziye kusetirika, kupunguza uchukuzi,
Pasafi ukaviweka, vilivyo na uchokozi,
Nawe ukapumzika, kuvuta safi pumzi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Wenzetu wanasifika, choo kwao matanuzi,
Chooni akishafika, huwa hafanyi ajizi,
Hakika hupumzika, akawa kitu hawazi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Kwingine si Afrika, chooni wanabarizi,
Hekima zikachmbika, vilokuwa hawawazi,
Na ujumbe wakaweka, uende kwa wateuzi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Yabidi kubadilika, vyoo tupate kuenzi,
Bila'vyo kuheshimika, itakuwa si saizi,
Yapo mengi kufanyika, ili tuipande ngazi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Kama nyumba ni mashaka, makazi ni kama zizi,
Vipi choo kujengeka, vyenye thamani azizi,
Watu watatosheka, kustawisha mizizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Hapa kwetu Afrika, hawawazi viongozi,
Wao wamesharidhika, kwa o vyoo i tailizi,
Sisi kutostaarabika, waona yetu saizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Wengi wao wanshafika, mengine hawayawezi,
Wabebwa kuzoeleka, wala hawafanyi kazi,
Wananchi wanateseka, wao kwao wabarizi,
Choo si pipa la taka, kikiziba kuna kazi !
Sunday, September 19, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment