Wednesday, September 15, 2010

Somo lipo vijijini

Nchi yetu kuendelea, vijiji budi kukua,
Haya tunayoyalea, tunakokwenda kubaya,
Vijiji vinadumaa, huku miji inakua,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Mtume hajatokea, vijijini kwenda kaa,
Darasani kuingia,maisha yanavyokua,
Kisha atapoelewa,vitani kuja ingia,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Mengi akiyagundua, shahada ataikwaa,
Utafiri kuzindua,tatizo lilipokuwa,
Na majibu maridhia,kichwani yakatulia,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Barabara zapotea,kusikokuwa na njia,
Nyoka walikojaa,sumu wanaotupia,
Pasipo pakutokea,vipi soko kufikia,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Maji ni ya kuchimbua,kama madini watoa,
Kote tope yamejaa,wahofu kuyatumia,
Wao wanywa, kufulia,ndicho walichojaliwa,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Nchi yazidi kukua,huku maji yapotea,
Bomba zinang'olewa,mifumo imechakaa,
Sasa kazi imekua,maji kujitafutia,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Umwajiliaji hadaa,wahandisi ruia,
Ni vipi utajiundia,kitu bila fundi kua,
Nchi bado imezubaa,twashindwa kujitegemea,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Shule zimetapakaa,walimu wamepotea,
Ujinga tunaulea,karne inayoingia,
Huko nje twajivunia,tumeshapiga hatua,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Watu bado kujijua,ni nani wa kuwaokoa,
Pipi wakishapatiwa,waona wamefikiriwa,
Vyama vingi wadhania,damu vitakujawatoa,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Hawajui demokrasia,kazi ni kuwapigania,
Ukiritimba kukataa,chama kinachowalemea,
Katiba mpya kutwaa,viongozi kuwafua,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Umeme haujaingia,kama waja hatujajua,
Giza linapoingia,ndio mwisho wa dunia,
Sayansi inaviambaa,vijiji vinasinyaa,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

Wenzetu wanaelewa, sola wanazitumia,
Miradi wameamua, nyumba zote kuwa na taa,
Sisi gizani twabakia,porojo twashangilia,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.


Misaada inatolewa,juu kwa juu yaliwa,
Siasa zatapakaa,na ushirikina pia,
Watu mengi wachelea,vigumu kujikomboa,
Somo lipo vijijini,wala sio ugenini.

No comments: