Sunday, October 7, 2012
Wakati nakuchukua
Ajabu haijakuwa, kuifungua tabia,
Mbona hayo nikijua, subira nikaamua,
Vazi nilishakuvua, ngozi ya mbuzi ukiwa,
Wakati nakuchukuwa, nilikuwa nakujuwa !
Dawa ulizotumia, mbona nilishaanguliwa,
Ushirikina nazaa, kwangu ni usioingia,
Ila ninachoamua, mwenyewe ninakijua,
Wakati nakuchukuwa, nilikuwa nakujuwa !
Kuteka ulidhania, mateka umepatia,
Mfukoni kunitia, na amri ukazitoa,
Nami nikikuitikia, ukadhani wayajua,
Wakati nakuchukuwa, nilikuwa nakujuwa !
Muda nilikuachia, upepo wanipepea,
Subra sikuachia, mvumilivu nikawa,
Wala sikukuchimbua, kukutafuta ubaya,
Wakati nakuchukuwa, nilikuwa nakujuwa !
Siku ninaingojea, kamba kujaachia,
Salama itapokuwa, kwa wana wanaokuwa,
Pembeni kujiangalia, na Molal nikamrejea,
Wakati nakuchukuwa, nilikuwa nakujuwa !
Pembeni kujiangalia, na Mola kumrudia,
Ndiye amenifungua, haya ninayoyajua,
Shukrani kuzitoa, uchamungu naamua,
Wakati nakuchukuwa, nilikuwa nakujuwa !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment