Wednesday, October 31, 2012
KUTONUNULIWA
Wahariri mashujaa, nienzio Tanzania,
Nyaronyo namkumbatia, siwezi nikamuachia,
Mkataa kununuliwa, ni mhariri shujaa,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Wasiokuwa na njaa, vya watu wakababia,
Rahisi kununuliwa, wachovu kuwanunua,
Dhuluma wakailea, kiyama kuyajutia,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Dini sintoangalia, kote wananunuliwa,
Roho naiangalia, wito inayoitikia,
Haki kuisimamia, si shetani kumfaa,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Hawa kwangu ni shujaa, kwa nyingi huba na hawa,
Ninawapenda radhia, na heshima naitia,
Lao nitalisikia, na yao kujisomea,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Waongo waliokuwa, bwana kutumikia,
Kama mbwa kuja kuwa, ovyo wanajibwekea,
Hao kwangu udhia, hata kama nawazaa,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Kwangu kina malkia, ukweli wanaujua,
Haki wanaitetea, na wanyonge kuwafaa,
Ila wanaotumiwa, kwangu mimi changudoa,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Fakiri ninajijua, wapi pakusimamia,
Kesho nimeshachagua, leo ninaiachia,
Wangu wanaonifaa,njia yangu kufatia,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Njiani wanaorudia, kuritadi wafanzia,
Siwezi wavumilia, wala kuwaangalia,
Nahesabu mfu wawa, kitu hawatatufaa,
Wahariri ushujaa, nyie kutonunuliwa !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment