Sunday, October 7, 2012
Hali ya hewa
Kuna pepo na dhoruba, tufani nazo mvua,
Na isiyo shwari Ghuba, karibu isiyokuwa
Zikichelea msiba, unaowanyemelea,
Hali ya hewa si njema, udikteta wachipua ?
Kuna gharika mraba, Marikani yatokea,
Obama alikoziriba, na waliomtangulia,
Hakitojaa kibaba, kwanza wao watatwaa,
Hali ya hewa si njema, udikteta wachipua ?
Urani ina janaba, tohara wapakazia,
Kwa wajinga wanaimba, nyimbo wasizozijua,
Ndotoni wakiwakaba, kizazi kukichimbua,
Hali ya hewa si njema, udikteta wachipua ?
Twashindwa vyoo kuziba, uranium kuchimbua?
Hiyo haijawa shaba, imewazidi tamaa,
Twautafuta msiba, kwa wenigne kwenda kuwa?
Hali ya hewa si njema, udikteta wachipua ?
Mabomu wakuziribwa, wengine hawatakuwa,
Kwetu wana ukuraba, ndiko watapoanzia,
Somalia wanayashiba, sisi ni kuyangojea,
Hali ya hewa si njema, udikteta wachipua ?
Kisipotosha kibaba, ukawa walia njaa,
Hautokuja ubwabwa, mauti huweza ingia,
Mikoba ameibaba, ya roho kuja kutoa,
Hali ya hewa si njema, udikteta wachipua ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment