Monday, October 15, 2012

V I J A N A L E O T A I F A



LAITI mkiamua, taifa leo vijana,

Hatua mtachukua, uoza kwondokana,

Nchi mkaifagia, kila kitu mkasana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Nchi inawangojea, kutumikia vijana,

Ndani mliochimbiwa, mso kitu cha maana,

Na nje mliokimbia, kuukataa utwana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Hamsini kutumia, sisi sasa si vijana,

Uzee unaingia,twafanana kama jana?

Kwa kuwa tunaachia, nchi inaumizana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Kazi tele zimejaa, tunaiona hiyana,

Ya kwanza yakuanzia, ni nyumba kujengeana,

Vijijini kuingia, kwa hali tukapambana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Wazee wanangojea, sadaka kupatikana,

Vijana ninawajua, Pongwe na Kimanzichana,

Nyenzo mkisaidiwa, nyumba zitaonekana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Na maji nayo pia, yaweza kupatikana,

Akili tukitumia, tukazingeneza zana,

Hizo za kununuliwa, ndizo zinazotubana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Miaka tulofikia, ni ya kutengeza zana,

Zote tunazotumia, maji yatapatikana,

Zoezi likaendelea, bila ya kukwamishana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Hadithi ukisikia, kukwama kupatikana,

Ni zana tumefulia, twangoja zitoke China,

Hali tukijitambua, kuunda yawezekana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Trekta ninajua, kuunda si kazi sana,

Moyo ndio watakiwa, na maono kuyaona,

Ombaomba kuzoea, hiana twafanyiana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Ardhi tutaifukua, tuweze kulima sana,

Chakula kujipatia, na kingine kuuuziana,

Marikani na Asia, nja tukatlizana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Uvuvi tunafulia, hapa pwani tunaona,

Samaki twashindwa vua, kwa udhia na hiana,

Misiri wameamua, jangwani wanapatikana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Misiri sasa wavua, jangwani kuna amana,

Yametuzunguka maziwa, sisi twasimangana,

Bahari twaiambaa, twavua pasipo zana ?

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Yote ukiangalia, uzee ndiyo hiana,

Kwaisha kufikiria, kwabaki kukimbizana,

Urais kufatia, haya, aibu hatuna,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Leo nimedhamiria, watu kuwachamba sana,

Utoto wanatutia, na upofu wa kutoona,

Wanaizuru dunia, hawana wanalovuna?

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Balozi tukiamua, hao wakawa vijana,

Elimu wataivua, na mbinu zenye kufana,

Wazee wajikalia, pipiefu kuivuns,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Balozi tukiachia, wakatawala vijana,

Ujuzi watahukua, kuja jenga mengi sana,

Nchi iwe yakimbia, si maktaimu kufwatana,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Wazee wang'ang'ania, tija wasipoitia,

Tukazidi kutambaa, badala ya kukimbia,

Ni udhia imekuwa, mwishowe unatakiwa,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Vijana ukiwalea, nyumba mnawaachia,

Waweze jisimamia, na hatua kuchukua,

Ya kwale wakiathiriwa, huja nyumba ikavia,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Vijana mmetimia, kwa wingi mmefikia,

Taifa mmeshakua, nchi inawasikia,

Hii ni demokrasia, idadi mshatimia,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !



Wenyewe mkizubaa, nchi watawaharibia,

Kifuu kitabakia, nazi nayo isokuwa,

Hata dafu maji kuwa, afadhali ingekuwa,

Vijana leo taifa, sio taifa la kesho !

No comments: