Monday, February 20, 2012

Waongo wakiondoka

Kila jambo linaanza, na kisha likaishilia,
Hawa waliyoyaanza, nayo yatamaliziwa,
Giza walilotutia, nalo likaondolewa,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Na wanaotuhadaa, tamati itafikia,
Chini waende kukaa, machoni wakapotea,
Na mwisho ndipo huwa, wakaacha kuwajua,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Kila ukitoa dua, Mola anaisikia,
Vingine kufikiria, mja waenda potea,
Hapo hapo shikilia, majibu kuyangojea,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Mengi watajifanyia, kwa haki kuzinunua,
Vyote ataporomoa, mkuu aliyekuwa,
Siku akizimia, kwa dua kuwasikia,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Usipoyashuhudia, mwanao atajionea,
Wakati ukifikia, hakuna wa kuzuia,
Ndivyo inavyokuwa, toka dunia kutua,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Wasiwasi kutokuwa, majibu hayatapotea,
Dakika inangojewa, saa iliyopangiwa,
Huyu mwenye kutimia, hakuna asilojua,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Hurithi wasiokuwa, kizazi kujimegea,
Kwa ajabu zake njia, wewe wabaki shangaa,
Ndivyo ilivyo dunia, na hizo ni zake njia,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Si kila kinacholiwa, tumboni kitaingia,
Ardhini huishia, kingi kinachozaliwa,
Na ndivyo inavyokuwa, ajabu yake dunia,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Sio tu kwa raia, hadi na waheshimiwa,
Gaddafy ungemjua, huachi msikitikia,
Kila alichoambulia, sasa mchanga keshakuwa,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

Na wengine walokuwa, leo wameshafukiwa,
Waliitaka dunia, lakini imewakataa,
Yenyewe inabakia, hakuna wa kubakia,
Tutashangilia siku waongo wakiondoka!

No comments: