Monday, February 20, 2012

Dhuluma itapungua

Kila jambo linaanza, na kisha likaishilia,
Hawa waliyoyaanza, nayo yatamaliziwa,
Giza walilotutia, nalo likaondolewa,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Wote wanotuibia, tamati itafikia,
Chini waende kukaa, machoni wakapotea,
Na mwisho ndipo huwa, wakaacha kuwajua,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Kila ukitoa dua, Mola anaisikia,
Vingine kufikiria, mja waenda potea,
Hapo hapo shikilia, majibu kuyangojea,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Mengi watajifanyia, kwa haki kuzinunua,
Vyote ataporomoa, mkuu aliyekuwa,
Siku akizimia, kwa dua kuwasikia,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Usipoyashuhudia, mwanao atajionea,
Wakati ukifikia, hakuna wa kuzuia,
Ndivyo inavyokuwa, toka dunia kutua,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Wasiwasi kutokuwa, majibu hayatapotea,
Dakika inangojewa, saa iliyopangiwa,
Huyu mwenye kutimia, hakuna asilojua,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Hurithi wasiokuwa, kizazi kujimegea,
Kwa ajabu zake njia, wewe wabaki shangaa,
Ndivyo ilivyo dunia, na hizo ni zake njia,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Si kila kinacholiwa, tumboni kitaingia,
Ardhini huishia, kingi kinachozaliwa,
Na ndivyo inavyokuwa, ajabu yake dunia,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Sio tu kwa raia, hadi na waheshimiwa,
Gaddafy ungemjua, huachi msikitikia,
Kila alichoambulia, sasa mchanga keshakuwa,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

Na wengine walokuwa, leo wameshafukiwa,
Waliitaka dunia, lakini imewakataa,
Yenyewe inabakia, hakuna wa kubakia,
Utajafika wakati, dhuluma itapungua!

No comments: