Hawaachi kuzuzuka, wanaozuka kwa shani,
Sanaa wanapovuka, hudhani wana thamani,
Wajione watukuka, nyumbani na mitaani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Kichwani yakishafika, wengi huwa ulevini,
Wajione wamefika, nao bora duniani,
Wakasahau hakika, hapa tuko mitumbani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Akili huwalipuka, wakawa ni majinuni,
Wakafanza ya dhihaka, wakacheka wanandani,
Washeshimu na rika, kujifanya baniani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Na shule ikipingua, usanii wawa guni,
Hawana watolojua, ila kidogo imani,
Wao wakajidhania, waifanya ihsani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Huchupa wakachupia, warudi abautani,
Huruka kujinyanyua, tahamaki wako chini,
Hupinda wakapindua, wasiwe barabarani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Hushika wakaachia, wakashika vya utani,
Kuja kushitukia, hakuna kitu mkononi,
Hujikweza wakakwea, ghorofa za kuelea,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Wakija kushtukia, huporomoka chini,
Moja ikija balaa, hujikuta nuksani,
Na waliowazimia, wawafanze afkani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Matope watu hupaka, huku eti wahisani,
Haya yakijasikika, hujikuta maruhani,
Nguvu kuja ishiwa, utu ukawa shimoni,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Kila kitu watataka, na kujipa ya thamani,
Wadharau walikotoka, wenyeji kuwa wageni,
Tapeli wanakotoka, wakaonekana shani,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Aya zimekusanyika, ametuonya Manani,
Dini wasioitaka, si fungu la duniani,
Na akhera wakifika, huwa wageni motoni,
Wanaozuka kwa shani, hawaachi kuzuzuka !
Sunday, February 19, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment