Saturday, February 18, 2012

Tijara ya madini haya

Busara imeambaa, ukubwa wameshalewa,
Haiwi haitokuwa, kwa wakati tulokuwa,
Faida nyingine kuwa, madini kuyachimbua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Dini anayeijua, uongo ataambaa,
Au yakijafikia, mapari kutwambia,
Uranium inafaa, sasa kwendakuichimbua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo!

Masheikh wakafatia, na tiki kwenda itia,
Na hawa huru kuwa, na sio wanaotumiwa,
Hakika tunawajua, ukweli wanaojua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo!

Hautatusaidia, maneno kuharishia,
Yatosha tunayojua, vingine haitakuwa,
Uwekezaji balaa, twaona unanukia,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !


Cha mbele kinshatembea, hakuna cha kurejea,
Maisha yamepungua, thamani hayatakuwa,
Na wanaoyachochea, hakuna asiyewajua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Chama kilicho na njaa, wanyonge chawahadaa,
Utu wasioujua, watu wema wajitia,
Afueni isokuwa, ndiyo inatarajiwa,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Wakati ninakataa, bado haujafikia,
Nusura haitakuwa, makaburi twachimbua,
Toka wanapoyatoa, hadi kwenda kuondoa,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Kisha twaenda changia, binadamu kuua,
Kwa pesa kujipatia, damu zilizomwagiwa,
Mola tunaamriwa, twapasa kweli kumjua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Heri litakalokuwa, mimi sintolikataa,
Na njaa ninaijua, ni mzazi wa tamaa,
Huweza ukakimbilia, liendalo kukuua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Nchi yangu ninalia, hatua uloingia,
NI kama umepagawa, na fikra kuepuliwa,
Tafakuri yalemaa, kama uliyechezewa,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

Namkabidhi Jalia, pekee alobakia,
Watu wangu kuwajua, na kisha kuwaangalia,
Baya kuwaepushian na wabaya kuumbua,
TIJARA ya uranium, kwa Tanzania ni kifo !

No comments: