Monday, October 24, 2011

Tujengeni kwanza kwetu

MOLA twamtanguliza,kwenye familia yetu,
Jina lake ni la kwanza,kabla maombi yetu,
Naye atatuongoza,sisi na kizazi chetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!


Twamshukuru Muweza, kujali kizazi chetu,
Kwake tuzidi pendeza,kumcha tusiache katu,
Kila kitu tutaweza,hata yasiyo saizi yetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Usafi kitu cha kwanza, iwe ni ibada yetu,
Uchafu kutokomeza, usikae ndani mwetu,
Udhu kuutanguliza, hii ndiyo kazi yetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Sauti kuipaaza, nje mlangoni mwetu,
Nje tukiwa twawaza, kwenda kweye mambo yetu,
Nuru kuitanguliza, na ije nyuma yetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Nuru iwe yaangaza, juu pia chini yetu,
Machoni kuipenyeza, na masikioni mwetu,
Mdomoni kuingiza, na ikae moyoni mwetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Izinge bila kukwazwa, kuzunguka miili yetu,
Itulinde bila kusaza, hisia na viungo vyetu,
Na tusiwe tunachowaza, ila ni sifa zake tu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Elimu twaokoteza, na hii ni kinga yetu,
Muda hatujapoteza, kutumia watu wetu,
Ujinga kuumaliza, iwe bora afya yetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Mashamba hatukukuza, hayakuwa mali kwetu,
Tufanze tunachoweza, tusiige ya wenzetu,
Biashara tukiwaza, iwe na manufaa kwetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

Sheria tukijifunza, tuwasaidie wenzetu,
Udaktari tukiweza, tuwatibu watu wetu,
Na yote tukiyafanza, tufanze kwa Mungu wetu,
Tujengeni kwetu kwanza, kisha tusaidie watu!

No comments: