Monday, August 20, 2012

Wenye pesa Tanzania




Fedha wameitamia, vifarana kuangua,
Wanasiasa wapewa, kesho kutoangalia,
Na vingine wagaiwa, upofu wakawatia,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Benki waliokwapua, na fisadi kuzipewa,
Madeni walioyatwaa, kwa ujanja na hadaa,
Na miradi kuizua, fedha zinakochanua,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Upofu wanawatia, wanaowashtakia,
Na wengine wanaua, kwa yao kukataliwa,
Shetani ajivunia, nchi kuja kuiua,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Matumbo wajishonea, mawili mawili wavaa,
Nafasi ikitokea, lingine huongezewa,
Jetha kawatunukia, hulka yake kutwaa,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Viongozi wanunua, mfukoni wakati,
Na kushoto na kulia, paredi wanatembea,
Ubepari waingia, hata nguo tutavua,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Na wakubwa wenye njaa, uziwi wameingia,
Zama walizozijua, leo wanafiikiria,
Mradi wajipatia, posho wanayopewa,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Hakuna wa kulilia, nchi yake Tanzania,
Kila mmoja kawania, ya kwake kupigania,
Mwalimu kutondokea, balaa zinazaliwa,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Hakuna alobakia, nchi kuigombania,
Kila mmoja awazia, ya kwake yakamfaa,
Na nchi kutochanua, mradi ajipatia,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Na Mola kawaachia, madhambi kujichumia,
Hadi milima ikawa, na toba kutoijua,
Hatimaye kuwavaa, kuwapa yao hidaya,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Ya ovyo wafatilia, ya utu kutoyajua,
Masikini wanalia, michezo washangilia,
Ushindi usiokuwa, wala neema kupewa,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Nchi wanajigawia, na keki ya Tanzania,
Wazawa pipi kupewa, shukrani wakatoa,
Yao yazidi lemea, washindwa kuyachukua,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

Siku ninaingojea, machozi kuyaachia,
Taulo ninaandaa, machozi kujifutia,
Tena la kuogeea, kubwa sana lililokuwa,
Wenye pesa Tanzania, wangojea kutawala.

No comments: