Monday, August 20, 2012

Vichanga haviyawezi

Vichanga haviyawezi

Vichanga vipe makuzi, uji na kisha ubwabwa,
Miezi inavyoenzi, vikaupata ukubwa,
Huvifanyia rawazi, kuja kushika makubwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Katika za kwetu enzi, vidogo vyapewa ukubwa,
Vilozea mchuuzi, na ugali vikakabwa,
Vikaachia machozi, kwa maneno wakagombwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Wanatumia hirizi, kuupata ukubwa,
Na njia bado ziwazi, msamba huja kuzombwa,
Kwenye videvu mchuzi, vindevu vikenda lambwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Ukubwa kama ujuzi, kiumbwe hilo kaumbwa,
Asiyekuwa mlezi, kawaidaye kukunbwa,
Mambo akayadarizi, kwa tambo zisizotambwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Huyafanza mazoezi, wachawi wasije bambwa,
Wakaruka kwa mizizi, na matawi kujigamba,
Kiazi hakiwi ndizi, hukikataa mgomba,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Vichanga haviyawezi, ya sasa ya kupambwa,
Uongo pia uwizi, ni nakshi za kurembwa,
Wazee wana ajizi, kwa njaa yao wafumbwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Yote yao maamuzi, na mtu mkono hulambwa,
Wakapewa upuuzi, kwa machimbo wakachimbwa,
Wakabakia doezi, vya watu kuja kuchambwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.


Namdiriki mjuzi, bwana aliye mkubwa,
Mmiliki mwenye enzi, na sultani mkubwa,
Anipatie malezi, na dunia kutorembwa,
Vichanga haviyawezi, mambo haya ya wakubwa.



No comments: