Monday, August 20, 2012

Hakuna dhambi ya chama



Wao wakikutumia, ubaya kutufanyia,
Kasumba kuiondoa, juu unahujumiwa,
Kiumbe unapoua, ni wewe uliyeua,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Ukinifanza kulemaa, chanzo nakutambua,
Watu kuwalingania, hofu hii wakatia,
Chombo ni kisafi huwa, damu inajifutia,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Dhambi inajifutia, kwa senti uanzopewa,
Ujinga ukitumia, motoni unajitia,
Nani wa kukuoa, hata wazazi hufulia,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!


Uongo ukiutia, dhambi unaichukua,
Hata kama wasemea, chama kilichokuwa,
Au serikali kua, sauti ya kutumia,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Uwizi ukituibia, hazina vilivyokuwa,
Benkini ukazitoa, wachache kwenda tumia,
Dhambi unaichukua, wala si chama tambua,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Uoza ukisifiwa, na wewe unalaniwa,
Haki ukiisiginia, nyayo zenda kuungua,
Kwa mawe ya mkaa, tayari umewekewa,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Wakubwa wakiamua, uliza na kulijua,
Haki lisilokuwa, kiumbe ni kulikataa,
Mzazi tumeambiwa, si kwa yote kumsikia,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Mzazi tumeambiwa, si kwa yote kumsikia,
Dhambi akituambia, ni budi kulikataa,
Mwenyewe kumuachia, njia zake akajua,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Uslama nausia, salama mtabakia,
Dini wasioijua, inafaa kurejea,
Kubaya mwaelekea, tiketi bure mwapewa,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Mazuri nawatakia, viumbe mojaliwa,
Wakakamavu mkawa, ila njia mwapotea,
Dhuluma manielea, dafrari kuchafua,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Kwa haki mkirejea, mavuno mtaachiwa,
Bora yaliyojaliwa, mikosi isiyokuwa,
Na wana mnaozawa, wasiwe wa kulaaniwa,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Yarabi nawaombea, hao wasiojijua,
Njia waliopotea, wabaya wawatumia,
Isafishe yao njia, peponi kuelekea,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi ni yako mwenyewe!

Yarabi nawaombea, hao wasiojijua,
Njia waliopotea, wabaya wawatumia,
Isafishe yao njia, peponi kuelekea,
Hakuna dhambi ya chama, dhambi yako bianfsi.


No comments: