Saturday, May 5, 2012

Huu ni wakati wetu



TWAPASHA wazazi wetu, miaka yao yaisha,
Walikuwa ni wenzetu, sasa wanajipaisha,
Ama nao kati yetu, ududu umeshakwisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Hii sasa mida yetu, ni nani anayebisha,
Viti vyenu, viti vyetu, twawaomba harakisha,
Na wanenu si wenetu, nasi twaanza zalisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Tuliwakopesha utu, mwatulipa magarasha,
Mwatugeuza viatu, tena vilivyokwishaisha,
Kumbe watu wana kutu, hilo latufadhaisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Mmeifyeka misitu, mkimaliza maisha,
Na kwa wenu ubutu, mwateta mwala maisha,
Sisi sio watukutu, ila kweli mwatuchosha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Mlitutia ufyatu, kwa dola kuritadisha,
Ibilisi kawa mtu, ndani mwamkaribisha ?
Hakika sio wenzetu, mmekwishatuonesha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Mtatutia vigutu, pindi tusipowakomesha,
Mioyo yenu kama chatu, ndio maana twaisha,
Kweu mchafu utatu, mliokwishauanzisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Wakowapi kina Tutu, chini wakawaketisha,
Wetu wana ukurutu, wanangoja kushibishwa,
Naona hamna kitu, wesha kabla ya kwisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Hawa wetu ni Mobutu, wangoja siku kuisha,
Wengine heri vifutu, waweza jislamisha,
Sio Moro si Kidatu, hawana cha kuzalisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Daladala ni matatu, jina wanabadilisha,
Mtu hawi ni kiatu, guuni ukajivisha,
Ndio hayao mwanakwetu, ama kwetu si maisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Lao haliwi ni letu, ila watufananisha,
Nisisngecheza upatu, msingi wangeanzisha,
Kwangu si heri mtutu, zogo sitaki anzisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Na makwao sio petu, vipi wajeniwezesha,
Nyumba iwe sio kitu, ila mali kuzalisha,
Hao nao sio watu, hili wangeshaanzisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Wametugeuza ratu, sangari kuikomesha,
Hakika maji matitu, jihadi wanaanzisha,
Binadamu bila utu, huwezi ukamtisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Na utu hauwi vitu, hili nawaelimisha,
Wito wenu sio wetu, haya tusipopitisha,
Sasa ni maisha yetu, ya kwenu yameshaisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Sasa ni maisha yetu, ya kwenu yameshaisha,
Acheni nafasi zetu, hali kuziimarisha,
Mkatoa tahyatu, sala mkahitimisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !

Malindi hadi Tumbatu, Shinyanga hadi Arusha,
Kwenye dhahabu na msitu, nia tunawakilisha,
Kiilichokuwa ni chetu, lazima kututajirisha,
Huu ni wakati wetu, zama zenu zimekwisha !




No comments: