Tuesday, May 29, 2012

Uongozi muflisi




Kila mtu akubali, kufilisika kubaya,
Ila ni kubwa ajali, viongozi kuishiwa,
Na ikawa afadhali, bora tu waliokuwa,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Hakuna yake mithili, viongozi kuishiwa,
Pakawepo idhiliali, hali watu kutojua,
Na Muumba kawa bahili, hataki tusaidia,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Zikabakia kauli, kila pahala zajaa,
Na vitendo ni muhali, maofisini wakaa,
Ikadhoofu hali, kwa dawa kutoijua,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Kakasirika Jalali, kwa maudhi yalojaa,
Watu wanyonga ukweli, na haki waiinunua,
Taabani binhali, ni nani mtamlilia?
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Watu wameacha sali, vimisi wafatilia,
Hiyo kwao ni asali, katika hii dunia,
Walikuwepo rijali, mbona waliozidia ?
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Walikuwepo rijali, mbona waliozidia ?
Uovu hawakukubali, kwa kesho kuihofia,
Kahfu kawanakili, hikma alojaliwa,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Walifanza bilkuli, maovu kuyakimbia,
Mola kawapa akili, shimoni wakaingia,
Wakalala hai hali, karne ikatimia,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Dunia kuikabili, miaka inshapotea,
Watu walipowasaili, ukweli wakagundua,
Mola wakamkubali, na kutubu shirikia,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Mola tukimrudia, hayo yote hutuvua,
Subira tukiandaa, muda hautapotea,
Siku itajaingia, nakama tukazivua,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

Ni wafu tuliokuwa, njiani tunatembea,
Maisha wamechafua, hakuna cha kujivunia,
Na motowakaribia, huku pepo wakimbia,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

NCHI naiombea, huruma sasa kupewa,
Balaa kuziondoa, na aibu ilokuwa,
Uhai tukaupewa, na uzima kuingia,
Kufilisika kubaya, lakini baya zaidi:
Uongozi muflisi !

No comments: