Saturday, May 5, 2012

Mwafrika mnafiki


Kiumbe haaminiki, wala hatelekezeki,
Hadhira isimlaki, bila ya kumhakiki,
Ni kubwa yake ashiki, ukwasi kuumiliki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Lini ikawa riziki, kiumbe anayemiliki,
Historia yashtaki, Maghairbi, Mashariki,
Kiumbe kutamalaki, kuizidisha hamaki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Ni kiumbe mabruki, lakini hafadhiliki,
Haliye huishtaki, hata kwao mushriki,
Na kwingine habebeki, uwezo hutaharuki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Anampenda Mali, awe mkubwa rafiki,
Ila yeye adhihaki, ucha mungu hautaki,
Na Mola hababaiki, kama yeye habebeki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Ni milki na milki, wamejaa wanafiki,
Na wasio taharuki, huwafukia handaki,
Wakawa hawazoleki, hadi Barru kuafiki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Nami hili siafiki, daima nawashtaki,
Hata kama sipendeki, sintokuwa mamluki,
Ni heri nikafariki, kwenda mbali kushtaki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Njia zangu za Sadiki, wala sio unafiki,
Mungu wengi sishiriki, hayo hayavumiliki,
Tawhidi namiliki, udhibiti nahakiki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

Yake hayatabiriki, mishtuko sidhihaki,
Nahofu haambiliki, isije kwangu riziki,
Nipate kilicho haki, uongo nisiafiki,
Mwafrika mnafiki, mwenyewe ajidhihaki !

No comments: