Tuesday, May 29, 2012

Vua gamba, vaa gwanda


VAA gwanda, vua gamba, kijana wa Tanzania,
Hamnao uchumba, na hawa wetu mabwana,
Kiuchumi ni wagumba, yetu katu hayatafana,
Vua gamba, vaa gwanda,  amka Mtanzania !

Wamezoea kukumba, sio watu waungwana,
Chokoraa waso kamba, wenyewe twaumizana,
Ngonjera kazi kuimba, wafanyacho sijaona,
Vua gamba, vaa gwanda, mpate vinara wapya?

Kijijini kuingia, utajiri kuibua,
Kwa kilimo kutumia, mbadala nayo pia,
Dunia ikatujua, na ukweli uliokuwa,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Viongozi twaishiwa, mafukara hatujawa,
Nchi wanaichezea, na muda unapotea,
Sasa tumejichokea, tunataka kuwatoa,
Vua gamba, vaa gwanda,  amka Mtanzania !

Vijna wataingia, bungeni wasiosinzia,
Tundu Lissu mithilia, Myika na Zitto pia,
Nchi haitotambaa, itaanza kutembea,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Ajuza, shaibu pia, wamekwishajichokea,
Kustaafu kwawadia, wanapaswa kuamua,
Twataka damu mpya, kuifaa Tanzania,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Kabla ya kufikia, uchaguzi yatakiwa,
Wananchi kutumikia, kazi wakashuhudia,
Na sio kuugombea, ukubwa wa kujitia,
Vua gamba, vaa gwanda,  amka Mtanzania !

Mitaani kuingia, kampuni mkazua,
Kwanini twachelewa, mbona za umma mwazaa,
Na wananchi nao pia, kuwa nazo watakiwa,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Akili kuzitumia, na ofisi kukimbia,
Wananchi nao kukaa, yao kuzungumzia,
Kila kitu kina dawa, mengine mwatutania,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Vijiji budi kukua, ya msingi kupatiwa,
Na bomba zikachanua, kila mahali kutiwa,
Wamechoka kuonewa, maisha kusumbuliwa,
Vua gamba, vaa gwanda,  amka Mtanzania !

Na umeme nao pia, kila nyumba kuingia,
Benki kuu kudaiwa, huduma kuzilipia,
Hadi nchi nzima ikawa, iko chini ya taa,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Wao walituambia, nyasi watatulishia,
Ili rahisi kupawa, ndege ya kusafiria,
Sisi tunawaambia, ni vingine itakuwa,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!

Sisi tunawaambia, mishahara twakataa,
Hadi njaa kuondoa, hapa kwetu Tanzania,
Waso tayari inafaa, waanze kutukimbia,
Vua gamba, vaa gwanda,  msidanganywe vijana!


No comments: