Tuesday, May 29, 2012

Z a m a z a k e z i m e i s h a !



Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Sasa ni kushindanisha, washindani watakiwa,
Na kataa kupotoshwa, vyama vingi si ubaya,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Anza kujitayarisha, hakuna kubaguliwa,
Wao wakikuzamisha, wengine hukuibua,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Na wenzako kuamsha, wajibu unatakiwa,
Hivi sasa ni kukesha, kulala ni kukataa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Hakuna wa kuzungusha, chao mapema kutwaa,
Sasa utawagoganisha, timu nyingi kuchagua,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Na wanaokuchokesha, kila jambo kungojea,
Sasa kuwachangamsha, kugura kuwatishia,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Magamba walojivisha, hawawezi kuyavua,
Hata wakijitingisha, kutoka litakataa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Gwanda wanaojivalisha, anza kuwachungua,
Kama hawajabebeshwa, wanaweza kukufaa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Njaa iliyowachosha, pia kuwatembelea,
Huenda kitu kuzusha, wakakushangilia,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Kadi wakikukopesha, unaweza kuingia,
Mkakati kuanzisha, nchi ukapigania,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Yamejaa mageresha, inafaa kuwatoa,
Mimi wakinichongesha, ufunguo nitakuwa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Wamejaa washawasha, hofu mwilini kuvaa,
Kidonda hukutonesha, ukabakia walia,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Wako pia mabahasha, wa mabara na visiwa,
Madudu ukianzisha, huweza kufanikiwa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Kuna kina jumlisha, na wengine wa kutoa,
Hesabu ukianzisha, wengi budi kusinzia,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Ni kutafuta maisha, mradi umeingia,
Dira, dari imezusha, nani anaona njia ?
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Vijijini kuamsha, ukweli wakaujua,
Yavia yao maisha, kimoja kushikilia,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Na mikoa kuivusha, wingi huu watakiwa,
Serikali kuanzisha, za mikoa kutufaa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Kimoja hakikatosha, kuitawala mikoa,
Madaraka kugawisha, lazima itatokea,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Waliopo wachemsha, hakuna asiyejua,
Kazi watu wafundisha, kazini wameshakaa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

Zama zake zimeisha, zama za chama kimoya !
Mengi sana yachekesha, na ukweli twaujua,
Mradi huu maisha, uongo vingine huwa,
Usikae katikati, sema uko chama gani !

No comments: