Saturday, May 5, 2012

Ubunge kujitolea



WAKATI umefikia, tume ninaiambia,
Kwa posho tu kuitoa, mishahara kukataa,
Mbunge akapatiwa, kaziye kujifanzia,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Ubunge wakimbilia, hata wasiotufaa,
Kisa kwenda kujilia, uhondo uliojaa,
Hili budi kuondoa, ikawa kujitolea,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Sasa wa kuulilia, hatokuwa mwenye njaa,
Mbali ataukimbia, mengine kujifanyia,
Wachache wakabakia, sisi wanaotufaa,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Kingereza wasojua, hapa hawatoingia,
Elimu itatakiwa, na ujuzi kujaliwa,
Na kisha mtu kupewa, kiwango alichokuwa,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Siasa zatuchafua, ujira mkubwa kutwaa,
Kiwango wasichofikia, wala kuwa na manufaa,
Hili sintoliridhia, kuliwa na wasojua,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Ajira nayo wakiwa, bora zaidi 'tkauwa,
Kampuni zao kuwa, ndizo zinazowafaa,
Na bungeni kuingia, iwe ni yao ridhaa,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Tundu Lissu wengi kua, bungeni waliojaa,
Sio wanaosinzia, pashioni kujilia,
Pembeni hao watakaa, na hawatovumiliwa,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Daktari watakiwa, kulipwa kilichojaa,
Maisha waokoa, sio hao kusinzia,
Nchi itaendelea, tukiishi kwa afya,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Walimu wanatakiwa, maslahi kupatiwa,
Sio wanaoongea, kitu wasichokijua,
Haya tukishapindua, ubabaishaji huvia,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

Bunge busara kujaa, na watu waliotulia,
Hekina wakatumia, wote wanoaingia,
Sana kuzungumzia, ya nchi yetu kufaa,
Wabunge wajitolee, kulipwa ni ufisadi!

No comments: