Saturday, May 5, 2012
Haukunipa sadaka
Haukunipa sadaka, niliponyoosha mikono,
Ulionyesha mashaka, nikasikia mguno,
Na nyuma hukugeuka, macho yaje makutano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Yangu yangelikufika, usingedhani kivuno,
Huku nilikovunjika, ni pamoja na kiuno,
Ni wapi pakusimika, ila hapa makutano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Mjinga sijaerevuka, akili zangu ni ngano,
Zamani nilisikika, hivi leo ni agano,
Mtu asiyehitajika, hivi ana mabishano?
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Kwenda kwangu kwa hakika, na wala si mapishano,
Rahisi lingejengeka, kbala mfarakano,
Nimeacha ya kuzuka, yatakuwa mshikamano?
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Nakuomba sikutaka, bila ya mivutano,
Ahadi yangu si shirika, usio ushirikiano,
Hapa nimepumzika, natazama wenye neno,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Hali yangu ya kizuka, inangoja mazikano,
Daraja siwezi ruka, hapo sina mlingano,
Kichwa kitanipasuka, kwa huo msuguano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Ndio mwisho ninafika, hapanalo tangamano,
Imekwisha Tanganyika, Tanzania sio neno,
Wameisha Waafrika, imebaki michuano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Yako sana nilitaka, kufuatia kisigino,
Nilidhani malaika, ningelkuwa na maono,
Hadi nikaweweseka, nilipotia tabano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment