Saturday, May 5, 2012

Haukunipa sadaka


Haukunipa sadaka, niliponyoosha mikono,
Ulionyesha mashaka, nikasikia mguno,
Na nyuma hukugeuka, macho yaje makutano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Yangu yangelikufika, usingedhani kivuno,
Huku nilikovunjika, ni pamoja na kiuno,
Ni wapi pakusimika, ila hapa makutano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Mjinga sijaerevuka, akili zangu ni ngano,
Zamani nilisikika, hivi leo ni agano,
Mtu asiyehitajika, hivi ana mabishano?
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Kwenda kwangu kwa hakika, na wala si mapishano,
Rahisi lingejengeka, kbala mfarakano,
Nimeacha ya kuzuka, yatakuwa mshikamano?
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Nakuomba sikutaka,  bila ya mivutano,
Ahadi yangu si shirika, usio ushirikiano,
Hapa nimepumzika, natazama wenye neno,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Hali yangu ya kizuka, inangoja mazikano,
Daraja siwezi ruka, hapo sina  mlingano,
Kichwa kitanipasuka, kwa huo msuguano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Ndio mwisho ninafika, hapanalo tangamano,
Imekwisha Tanganyika, Tanzania sio neno,
Wameisha Waafrika, imebaki michuano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

Yako sana nilitaka, kufuatia kisigino,
Nilidhani malaika, ningelkuwa na maono,
Hadi nikaweweseka, nilipotia tabano,
Nilinyoosha mikono, haukunipa sadaka !

No comments: