Tuesday, May 29, 2012
Utitiri haumwui
Hata kero hawawai, kwake mlalia mayai,
Katu hawajisumbui, wala hawawafikirii,
Na mchana hujiwahi, kwa vumbi kujistahi,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Ila sumu hiafai, wewe utakuwa mwui,
Dawa wangu simwagii, hili huwa ni jinai,
Nikazusha madai, kuupoeza uhai,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Utitiri hustahi, wakaangua mayai,
Vifaranga wako hai, nje wameshajiwahi,
Maji moto huzirai, utitiri ukiwahi,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Tena hapo hawakai, wameshaona nishai,
Huruka wakizirai, kwenda yao matlai,
Makazi kutanabahi, kuwa tena hayafai,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Kuku mama humuwahi, kwa dawa kumstahi,
Nao vifaranga hai, nyingi siwapulizii,
Hucheza wakafurahi, kero hawajionei,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Na jengine sinuni, yatosha kwao uhai,
Usafi siuachii, na maji kwa makarai,
Vinginevyo hawakui, kwa chema kujistahi,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Na majira yakiswihi, madhila hayarejei,
Nafuu ya jitimai, huwa tena haikawii,
Na shari haziingii, viumbe wasifurahi,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Matunzo hawakinai, viumbe madhali hai,
Na waja siwatanii, thawabu hutanabahi,
Ila wengi hawajui, wanyama hawaridhii,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Tamati ninaitii, zaidi siongezei,
Ukarimu wanidai, wingi tena haufai,
Nimekidhi maudhui, nyie zitoeni rai,
Kuku mlalia mayai, utitiri haumwui !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment