Tuesday, May 29, 2012

Hizi hapa bomba mbili


Bomba moja itaweza, kazi zake bomba mbili ?
Au ni kujishikiza, kungoja kitu kamili,
Kazi iweze kufanza, kwa haki na uhalali,
Hizi hapa bomba mbili, bomba moja itaweza ?

Kiasi chake hukuza, kwa idadi mara mbili,
Na kasi itafyonza, maradufu kulhali,
Na nguvuze za kuzoza, zinazidi mbavu mbili,
Hizi hapa bomba mbili, bomba moja itaweza ?

Wingi wake mwanagenza, ni kama pacha wawili,
Na mapipa huyajaza, yakazidi mara mbili,
Kuyabeba hutoweza, ila uwe na musuli,
Hizi hapa bomba mbili, bomba moja itaweza ?

Na pengine huchagiza, subira kama muhali,
Katikati kutokeza, pasiwe na afadhali,
Mkiacha yapooza, ni hasara mara mbili,
Hizi hapa bomba mbili, bomba moja itaweza ?

Kauli naikatiza, kwa maneno ni bahili,
Maudhui nimejuza, yanatosha bilkuli,
Mengina mtaagiza, tumieni 'imeili',
Hizi hapa bomba mbili, bomba moja itaweza ?

No comments: