Saturday, May 5, 2012

Ya Saudi Arabia



Usiwe nayo hasira, ya Saudi Arabia,
Watakiwao subira, kushindwa kuvumilia,
Uwe kama vile fira, jinyoka lenye kuua,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Na uongozi imara, hili jambo watambua,
Hawaitaki papara, za wenyewe kuumia,
Ramani huwa wachora, huku chini watulia,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Hakuna aliye bora, kiumbe wa kuzaliwa,
Mwaipandisha Hasira, ya Muntaqimu Jalia,
Hatowapa maghufira, juu mkijinyanyua,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Hii ni yangu bishara, mtawala kumwitia,
Aiepuke hasara, Ahadi kukusudia,
Na atoe manusura, mfungwa kumuachia,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Ninayaona madhara, kwa  ndugu kujiumbua,
Hayo yote si tijara, ni chuki yanayolea,
Na mkizikosa fikra, wote mtajapotea,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Dini yetu ni stara, magomvi kutozua,
Hasa kwetu walo bora, na ndugu tuliokuwa,
Wazandiki watuchora, hili wanashangilia,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Yabadilika majira, udugu kuukazia,
Dunia ni masihara, Islamu waumia,
Mkiitia mikwara, machungu yatasambaa,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

Tunataka uimara, na wala sio kupwaya,
Si nyoka vipi mwafura, au shetani mwamwachia?
Twawaombeni hadhira, tatizo kulitatua,
Au sumu utatia, pale isipotakiwa !

No comments: