Saturday, May 5, 2012

Lugha ngeni watumia



Lugha yetu yachukiwa, tena yadharauliwa,
Wapambe wlaliokuwa, nchi tumewaachia,
Kushoto waelekea, sisi twataka kulia,
Lugha ngeni watumia, wabakia ujingani !

Yabadilika dunia, jueni Watanzania,
Mzungu anafulia, kila mtu anajua,
Bado twawafuatilia, nasema tunapotea,
Sasa wanaajiriwa, makoloni yalokuwa,
Lugha ngeni watumia, uzungumze na nani ?

Sisi bado twasinzia, maajabu twategemea,
Naona huu udhia, siwezi kuvumilia,
Kweli ninasiimulia, haraka tujue waa,
Lugha ngeni watumia, unafeli mitihani ?

Kila kitu huzaliwa, na kufa  ni yetu njia,
Hata lugha nazo pia, wakati hujafikia,
Kihali zikaugua, na kufa ikafikia,
Lugha ngeni watumia, kwanini sio Kichina ?

Twatakiwa kuchanua, lugha nyingi kuzijua,
Maabara nawambia, za lugha zinatakiwa,
Huwezi jisomea, darasa halitofaa,
Lugha ngeni watumia, basi iwe Kifaransa !

Darasa sio radhia, maabara yatakiwa,
Sayansi hutumiwa, lugha nyingi ukajua,
Kusoma na kuongea, rahisi sana ikawa,
Lugha ngeni watumia, kwanini si Kiarabu ?

Bora teknolojia, hivi sasa zatumiwa,
Na katika wiki kadhaa, mtu lugha huijua,
Msada ukabakia, kila siku kujitia,
Lugha ngeni watumia, kwanini sio Kihindi ?

Maabara hutumiwa, kwa lugha tu kusomea,
Madarasa kubakia, lugha mama kutumia,
KIzazi kikajijua, na urithi kutopotea,
Lugha ngeni watumia, kwanini sio Kireno ?

Haya yanayotokea, wakubwa wanapotea,
Kasumba imewajaa, wamekuwa historia,
Yabadilika dunia, wao nyuma warejea,
Lugha ngeni watumia, wabakia ujingani !

Kilio ninacholia, mwatakiwa kuchukua,
Ujumbe ukaenea, na chetu kupigania,
Tusiachie oraa, ndio wawe mashujaa,
Lugha ngeni watumia, uzungumze na nani ?

Mkienda Malaysia, lugha yao watumia,
kadhalika Indonesia, lugha mama inang'aa,
Aidha nako Korea, si n yingine watumia,
Lugha ngeni watumia, unafeli mitihani ?

Na elimi imejaa, mizizi ilojaliwa,
Si ya ghibu kutia, bali kichwani yakaa,
Uvumbuzi waumua, kila ktu wagundua,
Lugha ngeni watumia, kwanini sio Kichina ?

Tumechagua kuua, lugha yetu asilia,
Hakika sisi majuha, najutia kuzaliwa,
Uwezo ningelikuwa, hili ningelikataa,
Lugha ngeni watumia, basi iwe Kifaransa !

Bahati twaichezea, shilingi tuliyopewa,
Chooni twaichezea, yaja sasa tumbukia,
Na ikisha tumbukia, tuone kitakachotokea,
Lugha ngeni watumia, kwanini si Kiarabu ?

Msishindwa wazamia, wapenzi msiokuwa,
Watu wawanyapaa, kwa chenu kukitetea,
Wala si kuwachukia, bali huruma kujaa,
Lugha ngeni watumia, kwanini sio Kihindi ?

Huruma kuwaonea, inafaa Tanzania,
Wameshindwa jitambua, waenda kusikofaa,
Bila idhini Jalia, utumwani twarejea,
Lugha ngeni watumia, kwanini sio Kireno ?

No comments: