Tuesday, May 29, 2012

Mtoto sina lugha yangu

Mtoto sina lugha yangu

Baba, pia mama yangu, lugha hawajaniachia,
Ni yatima wa wazungu, makombo nategemea,
Na kigumu kichwa changu, vya wengine kusikia,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Sijawahi mwona Mzungu, kuja kututembelea,
Nikifinyanga vyungu, ni wapi atanitokea ?
Na nikipata uchungu, yeye yangu atajua  ?
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Kama yangu ya uvungu, ninaweza kumwambia ?
Ulimi natia pingu, yangu lini kutambua,
Mswahili na majungu, mzungu na yake dunia,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Alichotugea Mungu, hivi tunakitezea,
Sijui mdudu chungu, bila ya kusaidiwa,
Wazoza ulimi wangu, chetu sina nianachojua,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Kadhalika na wenzangu, hawaijui mimea,
Limeisha letu fungu, hatuna cha kusomea,
Nchi naiona chungu, mambo yake kufifia,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Wanawajua Wazungu, wanyama tulojaliwa,
Huku kwetu ni mziungu, mwana gani awajua,
Ni chini ya yetu mbingu, lakini ibra wawa,
Ni yatima kwenye lug
ha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Vichwa tuumetiwa pingu, hatuwezi jitambua,
Hadhi yetu ya mabungu, elimu tunayopewa,
Cheo chetu sungusungu, wepesi kulaumiwa,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Kama tumelishwa kungu, kazi yetu kurembua,
Hata tupigwe marungu, vitu havitaingia,
Ila kama lugha yangu, nitaitesa dunia,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Mbona nasoma Kizungu, na sio Kichina pia,
Wanacho nini Wazungu, wengine wasichokuwa,
Na mimi mahaba yangu, ni Mchina kwenda muoa?
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Kingereza na Uzungu,  mimi nini wanifaa,
Hali ninamcha Mungu, naelekea Arabia,
Na dini ni langu fungu, zaidi nitajisomea ?
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Ndugu na shangazi zangu, mbona wako Malyasia,
Nikisomea Kizungu, watasikia Korea ?
Na wazulu si wazungu, mbona chao sijajua ?
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Moyo wetu, moyo wangu, mwatutesa Tanzania,
Lugha hiyo siyo yangu, kwanini mwang'ang'ania,
Mwatukausha mawengu, si watu wa kutulia,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Uturuki zama zangu, hata zenu mnajua,
Ni chao bila ukungu, na sasa wameshapaa,
Mkijitia uzungu, nini mwatusaidia ?
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Mafupi maisha yangu, ni kazi kujikomboa,
Muda huu sio wangu, mwazidi kuuchezea,
Hayaniishi machungu, kwa kushindwa endelea,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Kiswahili lugha yangu, ninaweza kutumia,
Zi wazi akili zangu, mengi sana yangeingia,
Iote mizizi yangu, mengine nikasomea,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Yakini wazazi wangu, digrii wangejipatia,
Kiswahili si uzungu, vyuoni vingetumiwa,
Na leo hii nchi yangu, hapa chini 'singekuwa,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Wamewanunua Wazungu, viongozi naambiwa,
Wataka sana kizungu, uchumi kutuibia,
Tuwe kama nyungunyungu, mvua kuitegemea,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

Aliyebakia ni Mungu, shida yetu kuijua,
Na wale wenye uchungu, lugha kuipigania,
Elimu iwe ni mbingu, tu ndiyo yatuzuia,
Ni yatima kwenye lugha, mwana sina lugha yangu:
Za wengine natumia,
Sikuzote kufulia!

No comments: