Tuesday, May 29, 2012
Atajua Kingereza ?
AJABU ilokuwa, ni wale wasiojua,
Ndio wanaopigania, Kingereza kutuoa,
Hali kukitumia utacheka na kulia,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Ilmu aliyopewa, mizizi haikupewa,
Sarufi kaitungua, kichwani haijakaa,
Na anachoongea, mwenyewe anakijua,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Maudhui huchafua, upukutike mkaa,
Na majivu kuingia, kama kuni katumia,
Wala hutomuelewa, si chake akililia,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Kiutu amefulia,na asili kaishiwa,
Na huyu kuendelea, na ije miaka mia,
Na bado ninakwambia, hapohapo atabakia,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Hawa mbona nawajua, katika hii dunia,
Walikuwepo India, hadi wakasanzuliwa,
Na Wahindi watumia, yao iliyojaliwa,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Hawa mbona nawajua, misaada walilia,
Na kila wanpoishiwa, rahisi kuzainiwa,
Lugha wakaichezea, kumbe ndio wanatuua,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Mwanzoni sikuwajua, hadi Makwetta kutua,
Mbeya nilipoingia, mjini kanitambua,
Akanipa historia, uongo nikaujua,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Kofia namvulia, ijapo kasahuliwa,
Shahidi kajipatia, yenyewe historia,
Labda waje kutia, uongo kusingizia,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Watu wa kuangalia, ishara hawajajua,
Nyuma wanaelekea, hali mbele tunatakiwa,
Huu mkubwa udhia, laiti wangelijua ?
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
India nashangilia, lugha yao kutumia,
Na wenzetu wa Korea, nyuma hawajabika,
Kadhalika Malaysia, na jirani Indonesia,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Vietnam nao pia, wajua yao dunia,
Filipino watambua, waukataa mzaha,
China ilitangulia, matunda yajivunia,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Kote ukiangalia, Afrika mtajua,
Lugha wanaotumia, isiyo yao ikawa,
Nadra kuendelea, tazameni Nigeriqa,
Hakijui Kiswahili, atajua Kingereza ?
Si mbwembwe na ubishhoo, na hana anachoweza?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment