Tuesday, May 29, 2012
Ishi na sisi tuishi
Namtaraji Munshi, kalamu kuwa aushi,
Niyaandike bilashi, yaliyochorwa nakshi,
Iwe yangu bakshishi, kwa wajao waandishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !
Uongozi si mazishi, si kikomo cha kuishi,
Kwangu ni uanzilshi, uhai wenye najashi,
Wakubwa ni matarishi, lingine hawafikishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !
Uongozi ushawishi, kama yalivyo marashi,
Nzi haukaribishi, ili kisicho tapishi,
Na mema hujaa pishi, na watu hawabakishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !
Haya ni utamanishi, kuyabeba kwa furushi,
Watu wapate bashashi, mazuri kuyanakishi,
Muda uwe hautoshi, katika wenu uashi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !
Mikono haurefushi, na miguu haiwashi,
Ukenda kwenye ushashi, uongo nao uzushi,
Ukawa ni hatarishi, kwa raia na majeshi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !
Ni kama mama mpishi, kaziye haimchoshi,
Hupika kila mapishi, na hakika si mbishi,
Na kitu hakibakishi, hulala njaa mcheshi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !
Hili haumfundishi, kazaliwa nayo pishi,
Mkononi ana dishi, na jengine haumpashi,
Kaumbiwa bishaushi, hadi siku ya mazishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !
Usingojee kuishi, baada yetu mazishi,
Yakanushe matamshi, tena bila tashwishi,
Hukugeuza uzushi, na kitu haurefushi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment