Tuesday, May 29, 2012

Ishi na sisi tuishi



Namtaraji Munshi, kalamu kuwa aushi,
Niyaandike bilashi, yaliyochorwa nakshi,
Iwe yangu bakshishi, kwa wajao waandishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !

Uongozi si mazishi, si kikomo cha kuishi,
Kwangu ni uanzilshi, uhai wenye najashi,
Wakubwa ni matarishi, lingine hawafikishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !

Uongozi ushawishi, kama yalivyo marashi,
Nzi haukaribishi, ili kisicho tapishi,
Na mema hujaa pishi, na watu hawabakishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !

Haya ni utamanishi, kuyabeba kwa furushi,
Watu wapate bashashi, mazuri kuyanakishi,
Muda uwe hautoshi, katika wenu uashi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !

Mikono haurefushi, na miguu haiwashi,
Ukenda kwenye ushashi, uongo nao uzushi,
Ukawa ni hatarishi, kwa raia na majeshi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !

Ni kama mama mpishi, kaziye haimchoshi,
Hupika kila mapishi, na hakika si mbishi,
Na kitu hakibakishi, hulala njaa mcheshi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !

Hili haumfundishi, kazaliwa nayo pishi,
Mkononi ana dishi, na jengine haumpashi,
Kaumbiwa bishaushi, hadi siku ya mazishi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi sisi tufe !

Usingojee kuishi, baada yetu mazishi,
Yakanushe matamshi, tena bila tashwishi,
Hukugeuza uzushi, na kitu haurefushi,
Ishi na sisi tuishi, usiishi ili tufe !

No comments: