Saturday, May 5, 2012

Neno toka mafichoni



WAJE juu na madege, na helikopta pia,
Wapambe kama nzige, anga na hii dunia,
Naweza nisiwaige, bado nikawanyanyua,
Neno toka mafichoni, linaweza kuwa dawa?

Hakika mfanywa bwege, neno lake akijua,
Yumkini wamroge, ndio chini  hutulia,
Ujinga tena afuge, kwake huwa ni nazaa,
Neno toka mafichoni, maskini kaamini?

Keshalikinai bunge, yake haliwezi jua,
Na japo mchafukoge, kuringa yake ridhaa,
Mpeni maji aoge, yake mkayaachia,
Neno toka mafichoni, mayatima waridhia ?

Watu hawajawa ndege,tunduni mkawatia,
Maishani muwafuge, uhuru kutowaachia,
Huja waje walichonge, sawia lililokuwa,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

Haijengwi kwa mizengwe, hii yetu Tanzania,
Haya bure mjivunge, mtakuja sanzuliwa,
Na wenyewe mjiroge, wengine kusingizia,
Neno toka mafichoni, linaweza kuwa dawa?

Demokrasia kikongwe, kila kitu inajua,
Elimu budi mlenge, msojua kurudia,
Burebure msijikoge, kaburi mwajichimbia,
Neno toka mafichoni, maskini kaamini?

Yapo yasiyo matege, twaweza zungumzia,
Na chama chenu mjenge,mambo mkafanikiwa,
Vingenevyo mringe,nasi tutawaangalia,
Neno toka mafichoni, mayatima waridhia ?

Twataka nchi mjenge,ushabiki twakataa,
Wabora wenu muige, uongo kutokuzua,
Nyoyo za watu mkonge, ridhaa mkapatiwa,
Neno toka mafichoni, linaweza kuwa dawa?

Ubabe budi mbwage, au utawaambua,
Watu ovyo msipige, madhambi mkayavaa,
Laana muwe vihongwe, mkaja kuachiwa,
Neno toka mafichoni, maskini kaamini?

Kirini ulegelege, ndani umeingia,
Gamba ili 'litokage', nusunusu kutoachia,
Na mkitaka 'mlindwagwe', wapo wa kushikilia,
Neno toka mafichoni, mayatima waridhia ?

Kengele sasa mpige, upya mpate zaliwa,
Ajizi msikoroge, sumu mkajinywea,
Ukweli msijivunge, vijan wawakataa,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

Kisa wao mwatenge, kuzaa na wa kutozaa,
Mkayaweka magenge, utu kujivurugia,
Kisha wenu muwafuge, wengine kuwaachia,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

Waona kanga na vitenge, mjini mkivigawa,
Vijijini muwakoge, uongo kuwaachia,
Na mbele wasisonge, karne yakaribia,
Neno toka mafichoni, wasonacho walijua ?

No comments: