Saturday, May 5, 2012

IBILISI KANAMBIA


Ahadi nimepokea, Lucifer keshanifaa,
Urais kuujua, nikaongoza dunia,
Na ukubwa kuutwaa, wateteme wenye njaa,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Nitabagua kwa nia,  kundini mwangu kujaa,
Kila mwenye kunifaa, ndio wa kumchagua,
Nao nisiowajua,  litakuwa bati baya,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Warembo nitachagua, Ikulu kuifagia,
Aidha kunipikia, na miguu kuangalia,
Masaji na kunichua, hayo sintoulizia,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Wahuni nitachagua, ulinzi kunifanzia,
Iwe panga ni pangua, hawi nami asokuwa,
Salama ni kukimbia, salama kisichokuwa,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Wazawa nitabagua, mali kujabarikiwa,
Ila wageni wafaa, rushwa nyingi wanatoa,
Hawa nitawaangalia, hata kama budi kuua,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Anasa nitachagua, aghali zilizokuwa,
Na vyombo kuvinunua, urahisi kuutia,
Na kitakapopungua, hatia mtu namtia,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Na nguo sintozivaa, tena nikzirudia,
Viatu nitavitia, kila aina vikajaa,
Marashi nitajitia, bei mbaya yalokuwa,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Sultani nitakuwa, hakuna wa kukataa,
Katiba nitabomoa, ya kwangu kujiundia,
Mlango ukifunguliwa, ukifufunga mzaha,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Dunia nitatembelea, hata kipofu nikiwa,
Mengi nitajionea, sina nitalochukua,
Umaskini yetu ndoa, misaada kujipatia,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

Msije kunizulia, hata nisiyoyajua,
Ninaganga yangu njaa, raia wajitegemea,
Mkate wasipopewa, keki nitawagawia,
Ibilisi kanambia, urais atanipa !

No comments: