Saturday, June 12, 2010

Wao wakipenda chao

Kwangu hilo sio tao, wala sio tegemeo,
Sio kama vipepeo, kwa mruko warukao,
Wala kwa rangi zao, na hizo safari zao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !


Nakusihi Samao, wewe mwenye milikiyo,
Nipe lako hifadhio, kwa dini niabuduyo,
Njia yangu lako chaguo, na wanangu wafuatao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !


Kwetu wewe kimbilio, kwa yote tutakayo,
Hukishi matarajio, kutupa yatufaayo,
Yaize matamaniyo, manufaa yasiyo nayo,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !


Hatuziwezi mbio zao, na mizigo wabebayo,
Na tukiwafuata wao, sio kati ututumayo,
Tunashika amriyo, hatuzishiki za kwao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !

Wache wapende wa kwao, hao wajidhaniao,
Wa kwetu si wa kwao, hao leo wawajuao,
Na wa kwetu uzao, ni wewe uwapendao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !

Wajinga ni waliwao, kwa wasiojua wao,
Upendo si mafao, wala chuki sio kilio,
Hutaka uyatakayo, hutumia upewayo,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !

Dua yangu mapitio, kwa wale niwafaao,
Thawabu wape wajao, pamoja na kinga yao
Ukirimu huu uzao, kuijua dini yao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !

Nimefikia kituo, na ujumbe ndio huo,
Wale mzingatiao, yawafae marejeo,
Wasiponifaa wao, utanipa unipao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !


Maajidi ni wanao, hawa tukuachiao,
Waongoze upendavyo, uwe mwema mwisho wao,
Wape lako kusudio, ndiwe uwajengao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !

No comments: