Kwangu hilo sio tao, wala sio tegemeo,
Sio kama vipepeo, kwa mruko warukao,
Wala kwa rangi zao, na hizo safari zao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Nakusihi Samao, wewe mwenye milikiyo,
Nipe lako hifadhio, kwa dini niabuduyo,
Njia yangu lako chaguo, na wanangu wafuatao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Kwetu wewe kimbilio, kwa yote tutakayo,
Hukishi matarajio, kutupa yatufaayo,
Yaize matamaniyo, manufaa yasiyo nayo,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Hatuziwezi mbio zao, na mizigo wabebayo,
Na tukiwafuata wao, sio kati ututumayo,
Tunashika amriyo, hatuzishiki za kwao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Wache wapende wa kwao, hao wajidhaniao,
Wa kwetu si wa kwao, hao leo wawajuao,
Na wa kwetu uzao, ni wewe uwapendao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Wajinga ni waliwao, kwa wasiojua wao,
Upendo si mafao, wala chuki sio kilio,
Hutaka uyatakayo, hutumia upewayo,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Dua yangu mapitio, kwa wale niwafaao,
Thawabu wape wajao, pamoja na kinga yao
Ukirimu huu uzao, kuijua dini yao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Nimefikia kituo, na ujumbe ndio huo,
Wale mzingatiao, yawafae marejeo,
Wasiponifaa wao, utanipa unipao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Maajidi ni wanao, hawa tukuachiao,
Waongoze upendavyo, uwe mwema mwisho wao,
Wape lako kusudio, ndiwe uwajengao,
Wao wakipenda chao, Badi penda kilo changu !
Saturday, June 12, 2010
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment