Saturday, June 12, 2010

Uongozi kama kazi

Haujesha usingizi, mjue wenu watani,
Kazi gani uongozi,mradi kono kinywani,
Na hawajitoshelezi,vipi wawaangalieni?
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Wewe hawakuwazi, rohoni bali mdomoni,
Mwageuzwa vijakazi, kwenye kura wabebeni,
Wakishaipanda ngazi,milele hamuwaoni,
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Wawatia bumbuwazi, kukejeli yenu imani,
Nanyi kama madowezi,ujanja hambaini,
Mwafikiria andazi,wenzenu wako angani,
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Hatuwaiti wapuuzi, lakini mna walakini,
Funza mwana hamfunzi, kujipachika kidoleni,
Uweje ni bazazi, yako yakose thamani,
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Maisha ni utelezi, mara hujikuta chini,
Na uliyempa ngazi,hutoa usiamini,
Ukakosa kiegemezi,shurti kukaa chini,
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Tunachagua machizi, twawapa kushika mpini,
Majembe na vifyekezi, twavishika kwa chini,
Wakivuta hawawazi,kinachotokea ni nini?
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Uongozi kama kazi, hii ajira makini,
Waweza kupiga dozi,siku nzima ofisini,
Na kukosa hauwezi,mshahara hutumiwa,
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Nawauliza wajuzi, jambo hili nambieni,
Jengoni wenye mizizi,na mitaa hawaioni,
Kweli hawa viongozi,au wasanii shani?
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

Uongozi kama kazi, nani awaongozeni,
Watu wataka mabenzi,sio kuwaokoeni,
Nyie kama nguvu kazi,lazima wawatumieni,
Uongozi kama kazi, mkono wenda kinywani.

No comments: