Saturday, June 12, 2010

Usijisumbue

Bure usijisumbue, huko sintoangalia,
Mwana usijishaue, kiwango hujafikia,
La leo usidhanie, kama la jana itakuwa,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!


Muda usijipotezee, utakalo halitakuwa,
Maisha usichezee, hili hukuandikiwa,
Bahati isikupotee, kwingine nenda kimbilia,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!


Hili usikimbilie, mwana litakukimbia,
Hapa usishikilie, gharika itakuzoa,
Matumaini yasijae, bahari ikajapwelea,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!


Karibu usisogee, usije ukaungua,
Macho usiyaachie, mwishowe utakujalia,
Mwili usiukaribie, peke yako kubakia,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!


Hili hakika silijue, mengine waweza jua,
Hili usilichukue, lazima utaachia,
Hili usilitegemee, halitakusaidia.
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!


Na pepo zinipepee, mie si mtu wa kukaa,
Popte usinitembelee, peke yako utabakia,
Moyo usiniachie, ukiwa utakuvamia,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!

Fanza moyo utue, kwa kutoroka tamaa,
Vitani usiingie, na silaha zilochakaa,
Ujibari ukimbie, kilema wajitakia,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!

Ili nisikuzuzue, nikabu ningelivaa,
Nahofu wasielewe, macho nje wanotoa,
Ngoja nijinyamazie, na uziwi kujitia,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!

Niache niendelee, na wangu mwenzi kukaa,
Sakura na uchague, utapata maridhia,
Si wako kamwe mie,moyoni hutonitia,
Usijisumbue bure, huna utachoambulia!

No comments: