Saturday, June 12, 2010

Kukuru kakara

Mtu wa tambo na visa, asikutie mkwara,
Watu hawa ni asusa, raha yao ni kukera,
Na wengi kama si tasa, basi hawana madhara,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.


Na wengi kama si tasa, wa mawazo na fikra,
Hawajawa mamajusa, kutabiri lilo bora,
Changamoto na fursa, kwao hazina tijara,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.


Hawaasisi kabisa, kazi kufwata bendera,
Njiani wanapapasa, hata mwanga uking'ara.
Na macho ni kupepesa, hawaioni ishara,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.


Wanatamani anasa, kwa ufisadi na ukora,
Kazi ngumu huzisusa, utadhani machotara,
Si ndizi ni kibubusa. hawachi kuja fura,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.


Hakika ninawaasa, hii iwe yenu sera,
Wasiwatie mkasa, watu wenye masihara,
Fungeni vyenu vitasa, barazani watadorora,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.


Mtenzi sina darasa, ningeliwapa ibara,
Masimulizi na visa, vya haokukuru kakara,
Vibaya walipojitosa, na kujikuta akhera,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.

Wafupi hutaka disa, urefu huwezi pora,
Pua ni ya kunusa, vipi wataka ipura,
Aliyejaliwa utasa, dawa yake maughufira,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.

Huwezi toba kususa, kuna Ibura kama za Sara,
Ufakiri sio posa, ndoa huweza kugura,
Jaha ikishakugusa, huwezi pata hasara,
Kukuru kakara ada, kwa madebe yaso kitu.

No comments: