Saturday, June 12, 2010

Nikifa sherehekea

Halijawa majaliwa, lile lisilojaliwa,
Pindo sio sawasawa, wala mstari kuwa,
Kama nilivyozaliwa, ndivyo nitavyojifia,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!


Nikifa sherehekea, pengine utajaliwa,
Milele hapa kukaa, hadi siku ya ukiwa,
Ahadi sikujaliwa, mie ni mpita njia,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!


Siku ninaichukua, kila ikija hatua,
Sina la kulikamia, lijalo ninaridhia,
Ndivyo nilivyozaliwa, vinginevyo sijawa,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!

4.
Hali yangu naridhia, sitaki kujishaua,
Nilicho nacho najua, ndicho ninachotumia,
Cha wengine sijajua, labda kipotee njia,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!


Edison atambua, haachi kunishangaa,
Nacho nilichokuwa, kidogo pia natoa,
Elimu na ya dunia, sijui kulimbikizia,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!


Sehemu kaibania, mashairi kupungua,
Aona namzulia, wa kutunga ni mmoya,
Sio raha ni karaha, sasa kwake nimekua,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!


Hawajui tangazia, cha ndani kilichokuwa,
Japo tumewaambia, wangali wanasinzia,
Wao jipya la kuzua, ukurasa kubania,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!


Na ndivyo walivyokuwa, binadamu nakwambia,
Wengi wa kukotoa, ila hawawezi toa,
Wengi wa kushangilia, ngoma wasioijua,
Nikifa sherehekea, ili uishi milele!

No comments: