Saturday, June 12, 2010

Ndoto njema

Usiku uliopita, ndoto njema niliota,
Jina lako niliita, kuitika hukusita,
Nilipo ulinifuata, napo tukaanza teta,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!


Kisha nilipokuvuta, ulikuwa kama uta,
Au nyuzi za gitaa, ukaja bila kubwata,
Shingoye ikafyata, uso wangu kuukuta,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!


Vidole niliviita, navyo vikanikumbata,
Mikono nikakamata, mwili wangu ukitweta,
Na midomo kuifuta, kwa vidole vikanata,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!


Jina lako nikaita, ukamwitika mwiita,
Pua yako nikakuta, na masikio kung'ata.
Kidevu nikakamata, na mashavu kuyakita,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!


Ndoto niliyoiota, surayo yameremeta,
Pumzi nilizozivuta, ujana nikaburuta,
Na mavune kuyasuta, nguvu mpya nikachota,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!


Kamba hii naivuta, sitaki kukukokota,
Njoo bila kusita, nyota njema inaita,
Wewe sio wa kupita, bali tujenge manyatta,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!

Nafaka nikizichota, fifi nitazipepeta,
Ungo nilioupata, kutumia sitosita,
Na kazi sintoiwata, ili na watu kuteta,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!

Ninawajuza wa Mvita, Kibarani na Taita,
Ninayataka makata, udi, uvumba mbatata,
Kunuiza vya kupata, kama asali na nta,
Ndoto niliyoiota,siamini, siamini!

No comments: