Saturday, June 12, 2010

Kumi na nane yatimu

Katujalia Alimu,imedumu yetu ndoa,
Na yetu mastakimu, hili yashuhudia,
Sasa ni ndugu wa damu, kaka na dada tumekua,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!


Jambo hili ni adimu, maisha yalivyokua,
Subira haikirimu, pupa mbele zimekua,
Wengi wana uhasimu, badala ya ngugu kua,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!


Umezidi uharamu, halali imekimbia,
Ulimi sasa ni sumu, ndoa nyingi unaua,
Wivu pia kutuhumu, navyo vinachangia,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!


Namshukuru Adhimu, toka kuwa mtarajiwa,
Hadi nikahi rahimu, tisini na mbili kua,
Nimemshika mwadhamu, nayeye kanishikilia,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!


Na machungu na matamu, yote tuliyachangia,
Hatuna cha kulaumu, Mwenyezi katujalia,
Twamwomba wetu Karimu, mbele kutuangalia,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!


Valentine baragumu, siku iliyobarikiwa,
Mimi na wangu dawamu, ndoa yetu ilikuwa,
Kama wema Waislamu, mashehe wakasomea,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!

Twamsihi Mukadamu, ya kwetu kutuafikia,
Tuwe watu wa salamu, wengine kutotegemea,
Ya kheri kutukasimu, wengine kuwasaidia,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!

Twakuomba ya Rahimu, isafishe yetu njia,
Twepushe na Jahanamu, kwa shetani kutukimbia,
Tupe yako ya Karimu, yaliyojaa ulua,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!

Kizazi chetu kidumu, katika sahihi njia,
Dunia isiwadhulumu, na wao kuitumikia,
Na jina langu lidumu, miaka itayofatia,
Kumi na nane yatimu, miaka yetu ya ndoa!

No comments: